Tuesday, May 3, 2011

Mei mosi Waziri asherehekea kwa kunywa kikombe

Na Thompson Mpanji,Chunya

Katika kusherehekea siku kuu ya wafanyakazi  mei mosi ambayo kitaifa ilifanyika mjini Morogoro,ambapo mgeni rasmi alikuwa Rais wa Jamhuri  ya muungano wa Tanzania,Jakaya Kikwete,huko wilayani Chunya  kuna  taarifa ya Waziri mmoja kuhitimisha  shamra shamra za sherehe hizo kwa kupata kikombe kutoka kwa mlemavu wa macho.

Akiongea na mwanablog hii Mkazi wa Kijiji cha Mbuyuni,Bw.Nico Haule amesema Naibu Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi,Mh.Philipo Mulugo jana alikuwa miongoni mwa wananchi waliokwenda kupata tiba ya  kikombe kutoka kwa  mpiga kura wake Mlemavu wa macho,Bw.Simon Mahela aliyedai  kuoteshwa na babu yake marehemu kutibu magonjwa yote sugu ikiwemo na ukimwi kwa muda wa siku 43.

Bw.Haule ambaye pia ni mdau wa masuala ya habari,amesema Bw.Mulugo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Songwe alikuwa mgeni rasmi katika sherehe za mei mosi ambazo zilifanyika Chang’ombe,Kata ya Mbuyuni,wilayani Chunya ambapo baada ya kuhitimisha sherehe hizo kwa kutoa msaada wa Sh.200,000  ili kusaidia shughuli za mei mosi ziweze kuendelea yeye na makatibu wake wa jimbo walikwenda kushuhudia  tiba hiyo na hatimaye kupata  kikombe cha tiba na hivyo kukonga nyoyo za wapiga wake  na kumuona ni mwenzao.

Mlemavu huyo wa macho anatoa tiba hiyo  kwa masharti ya matamio ya siku 43 bila kunywa pombe wala kufanya tendo lolote la ndoa amekuwa akitoa huduma kwa familia nzima kuchangia sh.500 ambapo siku ya Ijumaa watoto na wanafunzi wanakunywa kikombe bure.

Hata hivyo Bw.Haule amesema  viongozi kadhaa wa Wilaya ya Chunya akiwemo Mkuu wa Wilaya hiyo, Bw.Deodatus Kinawiro ameshafika kupata tiba ya mlemavu huyo wakati alipokuwa katika ziara za kikazi.

Mwisho.




Tuesday, March 29, 2011

Mashirika ya Caritas nchini yatakiwa kutokuwa mzigo wa majimbo ya kanisa katoliki

Na Thompson Mpanji,Mbeya
MASHIRIKA ya caritas nchini yametakiwa kujipanga vizuri katika utendaji wa kazi ,uwazi,uwajibikaji na ushirikishwaji ili yasionekne kuwa mzigo wa majimbo ya kanisa katoliki.
Mwito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Shirika la Caritas Mbeya,Bw.Edgar Mangasila ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mkutano mtandao wa mashirika ya Caritas kanda ya kusini (SHICANET)  wa siku moja uliofanyika katika ukumbi wa kituo cha malezi kwa vijana,kanisa katoliki,jimbo la Mbeya jijini hapa.
Bw.Mangasila amesema ili  Mashirika la Caritas yaweze kufanya vizuri katika utoaji wa huduma katika jamii na kuonekana yanafanyakazi vizuri, watendajike wanapaswa kufanyakazi kwa ushirikiano,kujipanga vizuri,kufuata miiko na taratibu za kazi na matumizi ya fedha yanayozingatia uwazi pale taarifa inapohitajika.
“Wafanyakazi wa Caritas mjitahidi msiwe mzigo wa majimbo,fanyeni kazi kwa uwazi na uwajibikaji siyo ibakie dhamira  safi tu bali  kila mtu anapohitaji kujuwa kinachoendelea akione,na hili ndiyo moja ya tatizo zinazofanya caritas nyingi zisipige hatua,kuna mashirika mengi kama Miserior ambayo yanapenda kufanyakazi nasi,hivyo tuzitumie fursa hizi,”alisema.
Ametaja sababu nyingine inayopaswa kuizingatia ni kuboresha mazingira ya watendaji,kutafuta mbinu za kutafuta fedha,mahusiano mema ya wafanyakazi na jimbo pamoja na kutekeleza  kwa muda muafaka shughuli zinazopangwa.
Mratibu wa SHICANET,Bw.Lufunyo Mlyuka amesema mkutano huo ni utaratibu wa mtandao kuwaunganisha wanachama  watendaji wa Caritas kutoka  katika majimbo nane ambayo ni Caritas Mbeya,Njombe,Iringa,Songea,Tunduru Masasi,Mahenge,Mbinga na Sumbawanga lengo likiwa ni waratibu kubadilishana mawazo na uzoefu,kuangalia changamoto,mafanikio  na mpangokazi wa Shicanet ili uweze kuwafikia wakurugenzi wote wa caritas.
Mwisho.

makala-maisha ya gerezani na uozo unaofukuta Na.3


Na Thompson Mpanji

......Japokuwa kwa mujibu wa maelezo ya wafungwa waliokaa kwa muda mrefu wakitumikia vifungo vyao wamekuwa wakisema  kuwa kwa miaka ya hivi karibuni kuna mabadiliko makubwa ya uangalizi na utunzaji wa mahabusu na wafungwa, lakini kwa upande wangu bado haikuniingia akilini baada ya kushuhudia mara kadhaa watu wakipigwa virungu kama mbwa mwizi.

Vitendo hivyo vimekuwa vikifanyika mara nyingi na maaskari wenye vyeo kuanzia staff sajenti kushuka chini( wasiokuwa na vyeo),nimeshuhudia laivu mara kadhaa askari anayeshughulika na mambo ya jikoni mwenye cheo cha sajenti maarufu kwa jina la gerezani kama mchokocho amekuwa akidiriki hata kuwapiga watu kwa kutumia mawe na vikombe bila kujali madhara yatakayotokea.

Vitendo hivyo vya upigaji ovy vimekuwa vikifanywa hata na wafungwa kuwapiga mahabusu jambao ambalo linafanywa ni la kawaida.

Tukiachana na virungu tunakutana na pointi  ya mizinga ,hii sehemu ni maarufu kwa ajili ya kukagua watu wanaoingia ama kutoka kwa kuamriwa kuvua nguo zote na kulazimishwa kuinama na kupanua makalio.

Zoezi hili limekuwa likifanywa kila kukicha bila kujali umri na wala haizingatiwi kama kuna baba na mtoto au mkwe hali inayoonyesha kuwa ni sehemu ya kudhalilishwa.

Imefikia wakati hata nguo mnazovaa ambazo ni safi zinatupwa chini na kukanyagwa kanyagwa ovyo na kuonekana hazina thamani yeyote na hauruhusiwi kusema lolote kinachotakiwa ni kufyata mkia.

Kwa ujumla utu  wa mtu ndani ya gereza unachukuliwa kuwa hauna thamani yeyote na kwamba kwa vile umeshakuwa mahabusu au mfungwa basi hauna haki ya kulalamika chochote zaidi ya ndiyo ‘bwana mkubwa’.

Hata unapoongea na askari hautakiwi kusimama nilazima uchuchumae hata ikiwa mtaongea masaa mawili bila kujali kama unaumia au umechoka.

Kwa ujumla jeshi la magereza bado linatumia  sheria na taratibu za kikoloni ambazo baadhi yake zimepitwa na wakati na hivyo kunahitajika mabadiliko yanayokwenda na wakati.

Ukiangalia vitendo vya manyanyaso na udhalilishaji vinavyofanyika kwa mahabusu kwa mahabusu au wafungwa kwa mahabusu hasa wakati wakutembelewa na ndugu vimekithiri.

Utakuta mfungwa anampiga mahabusu na kumkunja na kumsukuma sukuma huku ndugu yake akiwa anamwangalia na huku askari akisaidia unyanyasaji huo badala ya kukemea.

Ofisi ya utawala ndiyo ofisi kuu ya kufika na kusajiriwa na ndiyo ofisi inayotumika katika  kutoka lakini ofisi hiyo imekuwa ikiwafukuza watu kabla hata haujatoa shida yako imekuwa ni ofisi ya kuogopwa badala ya kukimbiliwa.

Admission ndiyo ofisi ya kuingilia na kutokea gerezani na ndiyo ofisi inayosikiliza matatizo yote ya mahabusu na wafungwa kabla ya kufika kwa Mkuu wa gereza  lakini haipo hivyo,wanabainisha wafungwa na maabusu ambao wamekuwa wakilalamika muda wote.

Pia kuna suala moja ambalo ni hatari sana ingawa linachukuliwa ni la kawaida lakini naamini ipo siku litakuja kuleta madhara makubwa kama wasemavyo waungwana ‘mzaa mzaa uzaa usaa’.

Mimi nakumbuka siku niliyokuwa natolewa polisi kituo cha kati kilichopo Mkoani hapa na kuingia ndani ya lori kubwa la kuchukuwa mahabusu maarufu kama karandinga tuliambiwa na polisi waliokuwa wakitulinda kuwa kama tunazo fedha tukabidhi maana huko tunakoenda kuna majambazi watakaotupiga ,kutukaba na kutunyang’anya fedha.

Nilijiuliza hao majambazi watatoka wapi ilhali tupo na maaskari,sikupata jibu na kwa vile sikuwa na kitu chochote chenye thamani sikuhofu.

Basi baada ya kuondoka hapo kituoni tulipitia magereza kuwachukuwa mahabusu waliokuwa wanakwenda mahakamani.

Alianza kuingia mahabusu mmoja baada ya mwingine na hapo walianza kutuangalia usoni na ghafla nikakuta wenzangu wanakabwa na kuanza kukaguliwa huku wakiambiwa kama una fedha toa wewe mwenyewe bila kupigwa.

Kwa kweli hali ile ilinishtusha sana na kuona mambo haya yamekuwa tuumachi yaani watu wanakabwa huku polisi wanaona na wasichukue hatua yeyote inashangaza na kusikitisha na iwapo hali ndiyo hiyo je huko mitaani haiwezekani polisi hawa hawa wakashirikiana na hao waharifu kufanya uharifu?.

Kama kwamba haitoshi baada ya kufika katika lock up iliyopo mahakamani hali ndiyo ilizidi kuwa mbaya zaidi baada ya wale vijana niliotoka nao Central kuanza kupigwa na kukabwa kooni huku wakilazimishwa waonyeshe walipoficha fedha.

Vijana hao walipiga mayowe ya kuomba msaada kwa askari bila mafanikio hadi sauti zilipowaishia kwa kukabwa kupita kiasi hadi hao wanyang’anyi walipomaliza kazi yao na kuwaacha vijana wakiwa hoi bin taaban.

Ukweli hali hiyo isipodhibitiwa watu wanaweza wakauana na nina kumbuka imeshawahi kutokea mahabusu kadhaa kupewa adhabu baada ya kufanya mchezo huo wakati karandinga halijatoka magereza.

Pia kuna mahabusu waliowahi kushtakiwa  katika mahakama ya wilaya kwa makosa ya kupaka kinyesi,kupiga na kujeruhi mahabusu wenzao.

Kutokana na hali hii  nina amini mamlaka pamoja na taasisi husika na masuala ya mahabusu na wafungwa zitafuatilia, kurekebisha  na kuboresha yale yanayowezekana kama ambavyo Mkuu wa gereza la Ruanda anavyodaiwa kurekebisha vifo vya mahabusu na wafungwa vilivyokuwa vikitokea kabla hajaanza kuongoza gereza hilo.

Aidha Jesh la magereza imefika wakati wa kurekebisha sheria na taratibu zilizopitwa na wakati na kuendelea kuimarisha mfumo wa mafunzo kwa wafungwa badala ya kuwa mfumo wa mateso ili mfungwa akimaliza kutumikia adhabu yake aende akawe raia mwema na mfano wa kuigwa katika jamii.

Hata hivyo katika makala ya mwisho   mwandishi wa makala haya atafanya mahojiano  maalum na Mkuu wa Magereza Mbeya,Kamanda wa Jeshi la polisi Mbeya,Hakimu mkazi Mkoa,Mwanasheria mkuu,msajili wa mahakama,Asasi zinazoshughulika na masuala ya haki za binadamu na sheria,Magereza mengine,Idara ya Ustawi wa jamii na baadhi ya wafungwa na mahabusu ili kujuwa hali ilivyo sasa na jitihada za kubadilisha hali za maisha ya wafungwa na mahabusu magerezani.

Mwisho.

makala-maisha ya gerezani na uozo unaofukuta Na.2


Na Thompson Mpanji
......Wanafunzi hao waliendelea kusema kuwa lakini walibahatika kuhama katika chumba hicho namba 12 na  kuhamia chumba namba saba ambapo walimkuta ndugu yao ambaye aliwasaidia kwa kiasi kikubwa kuepuka balaa hilo.

Hata hivyo Vijana hao waliiomba serikali kuzingatia kuwatenganisha watoto na watu wazima  na kwamba suala la kuwatenga katika chumba namba tano cha kulala watoto wadogo ndani Gereza hilo bado halisaidii chochote.

Pia wamewaomba wazazi kujaribu kutafuta njia nyingine mbadala itakayoweza kuwaadhibu ama kuwaonya watoto kuacha vitendo vya uharifu kuliko kuwapeleka magerezani hali inayopelekea kulawitiwa na kuambukizwa ugonjwa wa Ukimwi.

Vile vile wameiomba Serikali ibuni adhabu za kuwatia adabu kwa kuwaadhibu,udhibiti wa kijamii na makazi ya mpito ambapo wahalifu wadogo wawekwe na kupewa ushauri nasaha na huduma ya adhabu ya jamii.

Aidha Vijana hao wamewataka vijana kuacha tabia ya uharifu kwani madhara yake  ni makubwa baada ya kufikishwa gerezani kwani watashindwa kuhimiri misuko suko ya jela na hivyo watalawitiwa na kuambukizwa Ukimwi na hatmaye kupoteza maisha.

Tume ya Jaji Kisanga katika taarifa yake ya uchunguzi Magerezani iliyotolewa na idhaa ya kiswahili ya BBC mnamo April,19.mwaka huu ilithibitisha kuwepo kwa mlundamano na kutotenganishwa vijana chini ya miaka 18 hali inayochangia kuwepo kwa vitendo vya kujamiiana.

Hata hivyo imebainika kuwa asilimia kubwa ya watu ‘wanaocheza’mchezo huo wanakuwa wamefanyiwa mchezo huo kwa hali hiyo nao wanakuwa  na dhana ya kulipiza na kwamba mara kadhaa watu huwa wanarubuniwa siku ya kwanza waingiapo Gerezani.

Pia uchunguzi huo umebaini kuwa  asilimia 85% ya manyapara wa kifungwa ni wachezaji wa mchezo huo mchafu na hivyo inakuwa vigumu suala hilo kulidhibiti na kutokana na ushirikiano wao wa kutenda madhambi hayo inakuwa ni vigumu kesi za namna hiyo kufika kwa Mkuu wa Gereza.

Mara kadhaa kesi za namna hiyo zinaishia kushindwa kwa mtendewa kosa kwa kuonekana ni muongo mwenye nia ya kutaka kumuharibia cheo nyapara fulani na hivyo mlalamikaji uishia kupigwa virungu na kutokana na maaskari wengi kuwasikiliza hao manyapara basi wanaotendewa uishia kunun’gunika kimya kimya siku zote.

Pamoja na kukithiri kwa vitemdo hivyo lakini pia kuna jitihada za chini chini zinazofanyika katika kujaribu kukemea matendo hayo kama ambavyo Mwalimu mmoja wa dini wa kanisa la katoliki ndani ya Gereza ambaye ni mfungwa wa kifungo cha maisha ambaye pia ni nyapara Bw.Samweli Sanyage amekuwa akiwaonya  katika mahubiri yake mara kwa mara wafungwa na mahabusu kuacha kabisa mchezo huo.

Mkuu wa Gereza la Ruanda Dk. Malewa katika mikutano yake ya wafungwa na mahabusu amejitahidi kuwaonya mara kwa mara amekuwa akisema kesi nyingi zimekuwa hazimfiki.

Katika hotuba moja ya Agost,21,mwaka huu akizindua jezi za mchezo wa miguu ambapo ulifanyika mchezo baina ya mahabusu na wafungwa ambapo Dk.Malewa alisema kuwa michezo ni furaha na kwamba waache tabia ya kuingiliana na wajiadhari na ugonjwa wa ukimwi.

Dk.Malewa aliwaomba mahabusu na wafungwa kupima kwani dawa za kurefusha maisha zimeshafika Gerezani na kwamba kupima kunasaidia kuwa na uhakika na afya   na iwapo umeathirika usije ukamwambukiza mkeo pindi utakapo achiwa huru.

Mfungwa mmoja ambaye pia ni mmojawapo wa manyapara  Bw.Ahmed Dege katika mkutano mmoja alimuomba Mkuu wa Gereza kuingiza na kuruhusu kondomu zitumike ndani ya Gereza kwa kujikinga na maambukizo ya Ukimwi kwa madai kuwa vitendo vya ngono vimekithiri.

Ingawa Mkuu wa Gereza alijibu kuwa kuingiza kondomu ndani ya jela ni sawa na kosa la jinai, naye Mganga wa zahanati ya Gereza la Ruanda Bw. Oswald Hyera aliongezea kwa kusema kuwa  jitihada za kutoa elimu juu ya vitendo hivyo itaendelea kufanyika.

 Lakini bado kuna wafungwa na mahabusu wanaojali afya zao kwa kutumia kinga ya kondomu kama nilivyowahi kushuhudia mei,14 mwaka huu mfungwa mmoja jina namuhifadhi akifanya biashara ya  kuuza  kondomu moja aina ya salama kwa pande mbili.

Pia Januari,11 mwaka huu majira ya saa 4.30 asubuhi Nyapara mmoja wa Kifungwa alipokua akipekuliwa na ofisa mmoja wa Magereza mwenye cheo cha sajenti baada ya kutoka kufanya kazi za nje ya Gereza alikutwa na salama kondomu mbili kwenye ndoo ya plastiki.

Katika ukaguzi maalumu uliofanyika Septemba ,8.2004 Ofisa mmoja wa Magereza mwenye cheo cha nyota mbili aliokota  pakiti nne za kondomu aina ya salama zikiwa zimedondoshwa ardhini.   


Naye mahabusu mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Kyando alisema kuwa Serikali kwa kiasi Fulani inachangia kuongezeka kwa maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kutokana na  kuwaweka mahabusu muda mrefu bila sababu za msingi hali inayopelekea wake zao kushawishika kujihusisha na vitendo vya ngono ili kujaribu kupambana na makali ya maisha.

Uchunguzi umebaini kuwa iwapo Polisi wangetumia vizuri sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai (CPA) ya mwaka 1985 inayowapa wakuu wa vituo vya polisi uwezo wa kutoa dhamana kwa watuhumiwa wa makosa madogo madogo kama wizi wa kuku na uzururaji ingeweza kupunguza msongamano na hivyo kupunguza vitendo vya kulawitiana magerezani.

Kwa mujibu wa Kifungu cha 6(1) cha sheria no.7 ya mwaka 2001 ya tume ya haki za binadamu kinaipa tume mamlaka ya kutembelea na kukagua magereza lakini tume haijapita katika Gereza la Ruanda takribani mwaka mmoja  tokea Juni,2004 hadi Septemba,30.2005.

Ni maoni yangu kuwa taasisi zinazojihusisha na haki za binadamu zitembelee magereza mara kwa mara na wasiridhike na taarifa za  Wakuu wa Gereza wa Mikoa, (RPO) ama  wasiishie maofisini.


Pia Viongozi na Taasisi husika  mnapotembelea magereza sikilizeni maoni ya wafungwa na mahabusu moja kwa moja  vile vile watumishi wa  Taasisi hizo waingie magerezani kama mahabusu ili kufanikisha kufanya uchunguzi wa kina.

Magereza pia izangatie sheria na haki  za mikataba ya umoja wa Mataifa kuhusu hifadhi ya haki za binadamu na wajibu kwa jamii kwa mahabusu na wafungwa magerezani.

Watendaji hao wanapaswa kutambua kwamba haki za msingi za binadamu huathirika kwa kiwango kikubwa mtu anapotiwa Gerezani kwani uhuru wake uathirika,utu wake huchujuka na haki zake za msingi hukandamizwa

Idara ya upelelezi wa makosa ya jinai pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu zisicheleweshe kesi zikamilishe upelelezi kwa muda muafaka ili kuondoa mlundikano Magerezani na kwamba njia nyingine za adhabu zitumike mathalani wafungwa wanaotumikia adhabu ya vifungo chini ya miaka mitatu wapewe adhabu za faini, adhabu ya huduma kwa jamii.

Lakini pia waTanzania jifunzeni kuishi kwa amani,  utulivu na kufuata maadili mema,tafuteni njia mbadala zinazokubalika katika kujipatia riziki,rizikeni na kile mnachokipata na fuateni taratibu na sheria za nchi zilizowekwa.

Inaendelea…

makala-maisha ya gerezani na uozo unaofukuta


Na Thompson Mpanji,


KUNA msemo usemao “Ukistaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni”. Naukumbuka na kuuwaza msemo huu kila nikumbukapo mambo niliyoyashuhudia na baadhi kusimuliwa kuwa yamekuwa yakitendeka ndani ya gereza maarufu mkoani Mbeya, gereza la Ruanda.

Kwa wale ambao wamekuwa wakiishia kusoma masimulizi ya Sodoma na Gomora katika masimulizi ya vitabu mbalimbali vya kale, bilashaka wanaweza kuwa wamepata sehemu ya kuyashuhudia masimulizi hayo kwa macho yao kwa kushuhudia yanayojiri ndani ya gereza hili kongwe nchini.

Ni gereza ambalo pia litakukumbusha pia juu ya zile simulizi za samaki wakubwa kuwala samaki wadogo, tena kwa kutumia kila aina ya hila ili kutimiza malengo yao. Ukaifanikiwa kuingia ndani ya Ruanda, bilashaka utastaajabishwa na harakati, mbinu na kila aina ya hila ambazo hufanywa na binadamu (wafungwa kwa mahabusu)  za kutaka kulana bila soni wala huruma.

Nilipokuwa nikisoma vitabu mbali mbali vya dini vilivyokuwa vikielezea mambo ya Sodoma na Gomora, nilikuwa nikidhani kuwa ni hadithi tu, na nilipokuwa nikisikia juu ya uwepo wa watu wenye kushiriki matendo ya Ki-sodoma na Gomora, katika zama hizi, wakiwemo wanaume mashoga au wanawake wasagaji, bado ilikuwa hainiingii akilini.

Lakini ndugu yangu baada ya kukumbwa na mkasa ulionipelekea ‘niswekwe’ ndani ya gereza hilo, ambalo wenyeji wake (wafungwa wazoefu), wanaliita ‘Kigali’ wakiwa na maana mji mkuu wa nchi ya Ruanda,  nilyoyakuta huko yalinifungua kabisa macho na kunifanya nijione kama niko dunia nyingine na sio hii niliyokuwa nimeizoea.

Namshukuru Mungu sio tu kwa kuwa niliingia na hatimaye kutoka katika gereza hilo nikiwa mzima kiafya, bali pia kwa kuniepusha na tamaa ya kuliingia balaa hili la kujihusisha na biashara hii ya kishetani.

Si nia yangu kuwaelezeni juu ya kile hasa kilichosababisha mimi kujikuta niko Kigali, baada ya kukumbana na maafande wetu ambao ustaarabu kwao ni msamiati ambao hawakuwahi kujifunza katika maisha yao ya kusoma, bali zaidi kuwaelezeni kwa lengo la kuwaelimisha juu ya hali halisi ya kilichopo ndani ya gereza hili, kitu ambacho naamini kabisa ndicho kinachopatikana katika magereza yetu yote hapa nchini.

Kimantiki, magereza huwa ni sehemu ambazo hupelekwa watu ambao kwa namna moja ama nyingine wanakuwa wameshindwa kabisa kuendana na misingi au taratibu za kijamii za kimaisha, ikimaanisha kuwa magereza ni sehemu ambayo mwanadamu hutakiwa kwenda kujifunza ustaarabu kisha arejee katika jamii. Ndio maana hata jirani zetu Zanzibar sehermu hizio huziita Vyuo vya Mafunzo.

Hata hivyo katika Tanzania, jambo hili ni kinyume kabisa. Katika gereza la Ruanda kwa mfano, niliyashuhudia mengi ikiwa ni pamoja na jinsi mwanaume ‘anavyomsulubisha’ mwanaume mwenziye kinyume cha maumbile bila ya huruma.

Katika sehemu hii kikubwa ambacho kinachofundhwa kwa jamii iliyokusanywa hapo kwa lengo la kubadilishwa mawazo ni suala la kulawitiana, kiasi cha hata baadhi ya raia wa sehemu hizi kuwa wengine wamefikia hatua ya kuoana. Kuoana wanaume kwa wanaume? Hiki ndicho kinachofundishwa hata kwa wale ambao walisingiziwa na kukumbwa na balaa la kuswekwa ndani.

Ukimuuliza huyo ‘mlaji’kuwa ni kitu gani kinachompelekea kujizira kiasi hicho atakujibu uache kumfuatilia kwasababu wanawake hawapo humo gerezani  wataishije na namba (kifungo) ni ndefu? wakati huo anakuonesha  namba yake ya kifungo ambayo inaonesha anatoka mwaka 2040, hiyo ndiyo sababu wanayoiona ni ya msingi kwao.

Sasa unabaki kujiuliza kwanini mtu huyu hasivumilie na kujitunza ili pengine aweze kuishi kwa muda mrefu zaidi na pengine msamaha unaweza ukampitia na akaachiliwa  huru akiwa salama.

“Mimi hivi sasa nina umri wa miaka 55 na nimepewa adhabu ya kutumikia kifungo cha miaka 45,ebu fikiria kama kweli nikibahatika kutoka si nitakuwa sina nguvu kabisa kama sio kufia humu humu, kwanini nisimalizie nguvu humu humu jela?” alisema mfungwa mmoja ambaye alidai kuwa ana ‘watoto wa kijelajela’wanne.

Kwa wale wasiojua misemo ya magereza, Watoto wa kijelajela humaanisha sawa na wanawake huku uraiani, ikimaanisha kuwa mfungwa huyo yeye anawake wane hapo gerezani.

Mfungwa huyu ambaye jina namhifadhi, katika masimulizi yake kwangu, aliendelea kusema kuwa vijana wenyewe wanajipeleka kutokana na shida zao mbali mbali. Wapo wanaojiingiza katika matendo hayo kutokana na kutokutosheka na mgao wa kawaida wa chakula, wapo wanaotaka kupata sigara, unga,  bangi na wapo ambao hutaka kuvaa vizuri na kwamba yeye  huduma hizo zote anazimudu kuwatekelezea.

Pia imebainika kuwa maandalizi mabaya wa chakula  ambacho pia hakitoshi (pungufu ya gramu 500) kukidhi njaa kwa mahabusu na wafungwa ni sababu mojawapo inayochangia kuenea kwa tabia hii ya kulawitiana.

Kwa upande wa vyakula, magereza kuna utaratibu wa aina mbili. Kwanza kuna sufuria linalopikwa kwa ustadi wote ambalo linakuwa ni maalum kwaajili ya wapishi na malwatani ambao kiwango chao cha kawaida cha chakula, iwe ugali au chakula chochote huwa ni zaidi ya mara nne ya mgao wa kawaida wa wafungwa gerezani. Sio jambo la ajabu kumkuta mfungwa wa aina hii akiwa na ugali zaidi ya  gramu 2000 ulio mzuri na ulioiva. Pia  maalwatani hao wanakuwa na Mboga tofauti tofauti (samaki wabichi, mboga za majani, mayai na nyama)  iliyokaangwa kwa mafuta.

Aina ya pili ya vyakula ndani ya gereza hili kama ilivyo katika magereza mengi ni ile ya vyakula vya walalahoi ambao hupokea  ugali mbichi dirishani usiofikia hata gramu 500 pamoja na mboga yenye ujazo wa gramu 30 iliyochanganywa mchicha, maharagwe na dagaa bila kusahau konokono wadogo na michanga bila mafuta.

Nafikiri kutokana na hali hiyo utakubaliana na mimi kuwa hapo inawezekana kabisa ‘samaki mkubwa akammeza kwa urahisi samaki mdogo pasipo shaka yeyote na kwamba  chakula kuwa kidogo ndiyo sababu mojawapo inayopelekea watu kushawishika kujihusisha na vitendo hivyo.

Lakini pia kwa wale wenzangu  ‘machain smoker’ ambao wanapenda kuvuta sigara ama bangi wanakamatika kwa urahisi na kushawishika na vitendo hivyo na watu wa aina hiyo  wengi wao wamekuwa radhi kufanya vitendo hivyo vichafu kwa minajili ya kuwa na uhakika wa kuvuta kila siku.

Bei ya sigara moja iwe sportsman, sweet menthol ama club na kadhalika ni mapande mawili ya sabuni ikiwa na maana sh.100/- kwa maana kipande cha sabuni ya kufulia ambacho huku uraiani kinauzwa sh.100/- kwa jela thamani yake ni sh.50/- ambapo tumbaku au ‘Mbama’ kwa lugha maarufu ya jela inauzwa pande moja.

 Wapo watu wenye uwezo wa kuwagharimia kiasi cha sh.500/- kila siku watoto wao kwa ajili ya uvutaji mbali ya kuwanunulia matunda, vitafunwa kama chapati, maandazi ama kinywaji kama juisi za kwenye vipakiti..

Malazi ni moja ya sababu kuu inayowafanya watu washawishike na kukubaliana kulegeza masharti ya msimamo mkali wa kutojihusisha na biashara hiyo kwa mfano tukiachia vilago vilivyoishia Septemba,2004 na kuletewa godoro za sponji zenye urefu wa nchi sita na upana inchi mbili na nusu.

Godoro hizo zimewekwa 32 katika kila chumba cha kulala chenye urefu wa futi 40 na upana wa futi 15 lakini watu wanafikia kulala (kwa mfano novemba,28.2004 walilala watu  94,februari,2.2005 walilala watu 102) katika chumba kimoja  wakati huo huo kuna manyapara wa kifungwa watano katika kila chumba ambao wao kila mmoja analala katika godoro lake.

Mbali ya hao viongozi wa kifungwa kuna maaskari wa chumba cha kulala (maaskari cell) ambao wanakuwa watatu katika kila chumba cha kulala ambao nao kila mmoja anakuwa na godoro la peke yake la kulala na pia  viongozi hao wote wanakuwa na magodoro ya ziada kwaajili ya ndugu jamaa,’Warombo’ (yaani watu wanao ishi nao kwaajili ya manufaa fulani) pamoja na‘watoto wa kijelajela’.

 Kwa wastani jumla ya  godoro 16 zinakuwa zimeshamilikiwa na hivyo kubakia godoro 16 ambazo watu  watalundikwa hapo  panapoitwa kichakani au sensa kwa hiyo karibu watu 64 wanatakiwa walundikwe katika godoro16 zenye upana wa inchi mbili na nusu.

Ni matumaini yangu utakuwa umeshapata picha halisi ya ulalaji ndani ya jela   kiasi kwamba watu wanalazimika aidha kwa lazima ama kwa ridhaa yao wenyewe kucheza mchezo huo wa kishetani.

Kutokana na hali hiyo ndiyo maana kesi za ‘kunyatiana’kuingiliana bila ya ridhaa zinakuwa nyingi, japo huku uraiani hazisikiki mara zote.

Mfano kuna kesi ya wafungwa kunyatiana iliyotokea Januari,3.2005 ambapo mnyatiaji alipewa adhabu ya kufungwa pingu mikononi na miguuni kwa muda wa siku saba na baadaye alihamishiwa Gereza la kilimo la Songwe lililopo Mkoani hapa.

Lakini pia wapo watu wanaolazimika  kujiingiza katika biashara hiyo kukwepa ‘harasi’ za mara kwa mara kwa kupigwa na hao viongozi (Nyapara) na kusingiziwa sababu za uongo kwa maaskari jela kama vile kuwa na fedha ukapigwa kirungu mpaka uoneshe ulipoficha, umechukuwa chakula mara mbili wakati siyo kweli, ama utakuwa unachaguliwa kila wakati kufanya usafi na pia utakuwa unanyimwa maji hata ya kuoga.

Hiyo yote ndiyo mitego wanayoitumia wataalamu hao kuwanasa ‘watoto wa kijela jela na hatimaye kuwaweka katika himaya zao na kuwatumia kadri wapendavyo.

Pia wapo wale ‘watoto wa kijela jela’ wazoefu ambao wao  wamekubuhu katika fani hii hawa huwa hawana ‘wazee,’ wao huwa wanafanya mchezo wao wa chapu chapu  sehemu ya vyoo maarufu kama machemba na kumaliza shida yako kwa makubaliano ya pande nne za sabuni,10 ama 20. 

 Uchunguzi wa kina umebainisha kuwa huko chooni biashara hiyo huwa inafanyika muda wa mchana wakati mahabusu wanaenda kula na ndipo utakuta mwangalizi wa choo anaanza kufanya usafi wa kupiga deki na kuweka mpira wa kuzibulia kinyesi mlangoni (maarufu kama mchokocho) ikiwa ni ishara ya kutoruhusiwa mtu kuingia kwa muda huo ama kunakuwepo mtu anayezuia watu wasiingie kwa kisingizio cha kufanya usafi wakati siyo kweli.

Aidha imebainika kuwa vijana wanaoongoza kwa kujihusisha na vitendo hivyo ni pamoja  na vijana wa makabila wa Kinyiha wakifuatiwa na Wamalila, Wasangu na Wanyamwanga  na hii inatokana na wengi kutoka katika vijiji vya mbali na hivyo kuwa ni rahisi kudanganyika  ama kutishiwa.

Pia kanuni ya viwango vya kimataifa ya kuwatenga watoto na watu wazima haifuatwi katika gereza hili hali inayopelekea watoto kutomudu misukosuko ya vitisho vya kibabe na badala yake  kuishia kujiingiza katika biashara hii haaramu na hatari kwa pande ziote zinazohusika.

Kulikuwa na matukio mawili kwa mfano ambayo yalihusisha watoto walioshurutishwa na uzembe wa serikali yetu kutupia macho magereza na sheria za kimataifa za magereza kwa watoto ambapo katika tukio la kwanza mtoto mmoja wa miaka 13, aliyekuwa mahabusu Oktoba, 8.2004 alidaiwa kulawitiwa mara mbili na Nyapara mmoja.

Tukio hili lilikuja kubainika Oktoba18,2004 baada ya Mganga wa zahanati ya Gereza Dk.Oswald kuthibitisha, lakini kesi hiyo haikufika kwa Mkuu wa Gereza iliishi mikononi mwa Manyapara wa Kifungwa.

Katika tukio jingine Nyapara mwingine wa kifungwa alivuliwa cheo hicho na kuhamishiwa katika Gereza la Ileje kutokana na kumlawiti kwa nguvu na kumsababishia maumivu makali kijana mmoja mkazi wa Uyole mkoani Mbeya.

Hata hivyo Wanafunzi wawili ambao waliingia katika Gereza hilo kwa kutuhumiwa kuiba sh.40,000/- za wazazi wao walijutia kuingia kwao Gerezani kutokana na kutokuwa wasikivu kwa wazazi wao.

Vijana hao mmoja ana umri wa miaka 16 mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya Sekondari ya Mbeya Day na mwingine mwenye umri wa miaka 17 mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya Sekondari ya Igawilo ambao waliingia Gerezani Septemba,7 mwaka huu  walisema kuwa walisumbuliwa sana kwa nia ya kuwataka kimapenzi.

Inaendelea.....